
Afisa Mdhamini Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Mwalimu Mohamed Nassor Salim amekipongeza Kituo cha Elimu mbadala Wingwi kwa kutoa maarifa juu ya changamoto zinazoikabili jamii hali inayotoa hamasa kwasababu wanaungana na sera za nchi katika kuongeza fursa za kupata ajira.
Amesema hayo wakati wa ufungaji wa Mafunzo ya Siku mbili kwa Waalimu wa Kituo hicho yaliotolewa na Wakufunzi kutoka Tume ya Taifa UNESCO, katika Ukumbi wa Mikutano wa kituo hicho huko Wingwi Mkoa wa Kaskazini Pemba.
“Naamini kabisa kuwa mafunzo mliyoyapata yataboresha kwa kiwango kikubwa utendaji wenu wa kazi na kufanya kituo hiki kutekeleza kwa weledi jukumu lake muhimu sana la kuandaa vijana watakaoweza kujiajiri kwani jukumu mlilonalo ni kubwa sana kwa ustawi wa maendeleo ya nchi,” Amesema Mwalimu Mohammed.
Aidha amebainisha kuwa Mafunzo ya Elimu ya Ufundi Stadi yanagusa eneo muhimu sana la vijana, kwani vijana kupata elimu hiyo itawawezesha kuwa na aina mbali mbali za ujuzi katika utendaji kazi.