- Details
- 790
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla amesema kukamilika kwa ujenzi wa Skuli ya Msingi ya Ghorofa Kojani kutasaidia kuboresha sekta ya elimu kisiwani humo kutaondoa changamoto ya uahaba wa madarasa, walimu na vifaa vya kusomea na kusomeshea.
Akikagua jengo hilo linaloendelea kujengwa katika kisiwa cha Kojani Mhe. Hemed amesema katika kuhakikisha Sekta ya Elimu inaimarika katika Kisiwa cha Kojani Serikali itaajiri Walimu wazawa ambao watafundisha kwa ari na upendo ili kutatua changamoto ya uhaba wa Walimu Kisiwani humo.
Amesema kukamilika kwa Skuli hiyo wanafunzi watapata fursa ya kusoma katika mazingira mazuri pamoja na kuwa na vifaa kwa kisasa vitakavyowasadia kupata ujuzi wa masomo wanayopatiwa.
Amewanasihi Wazazi na Walezi katika Kisiwa cha Kojani kuachana na tabia ya kuwakatisha Masomo Wanafunzi wa Kike na kuwazesha badala yake wawahimize katika kusoma ili kupata Wataalamu wa fani mbali mbali ambao watasaidia katika kukiletea maendeleo kisiwa hicho na Zanzibar kwa ujumla.