Naibu Katibu Mkuu Utawala, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Ndugu Amos John Henock, amesema Wizara imeweka mikakati na malengo mahususi ya kupambana na vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na wasichana, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kukuza ustawi na nafasi ya mwanamke katika jamii.
Amesema licha ya wanawake kuwa na idadi kubwa katika maeneo mbalimbali ya jamii, ikiwemo skuli, bado wanakabiliwa na changamoto za kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi, kisiasa na kijamii.
Ndugu Amos ameyasema hayo wakati wa kongamano la siku tatu la kuwajengea uwezo wadau mbalimbali, wakiwemo Maafisa Elimu wa Mikoa na Wilaya, Maafisa Takwimu, Maafisa Ustawi wa Jamii pamoja na wadau wa Sheria, lililofanyika katika ukumbi wa Skuli ya Abeid Amaan Karume, Mwera, Wilaya ya Kati Unguja.
Amewataka Maafisa Elimu wa Mikoa na Wilaya kutumia ipasavyo mafunzo hayo katika kusimamia miongozo na taratibu zilizowekwa, ili kuhakikisha nafasi na haki za wanawake na wasichana zinalindwa na kupewa umuhimu unaostahili.
Amesisitiza kuwa ukatili wa kijinsia hauishii katika ubakaji pekee, bali unajitokeza katika maeneo na namna mbalimbali, ikiwemo katika maeneo ya utoaji wa huduma.
Aidha, amesema Wizara inakusudia kuanzisha dawati maalumu litakaloshughulikia masuala ya jinsia na wanawake, kwa lengo la kujenga uwezo wa kushughulikia na kufuatilia kesi zinazohusiana na masuala ya jinsia. Dawati hilo pia litashirikiana na Jeshi la Polisi katika kushughulikia changamoto zinazohusiana na dawa za kulevya, ukatili wa kijinsia na ajali za barabarani, ikiwa ni sehemu ya kuongeza uelewa kwa jamii na kupunguza vitendo vinavyoweza kuepukika.
Kwa upande wake, Afisa Elimu Wilaya ya Kusini Unguja, Ndugu Mussa Nahodha, amesema Maafisa Elimu wako tayari kuyatumia mafunzo hayo katika kuongeza uwezo wa kupinga vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na wasichana na kuhakikisha wanayafanyia kazi kwa weledi.
Amesema Maafisa Elimu ni sehemu ya kamati zinazoshughulikia masuala ya kupinga ukatili katika ngazi za Wilaya na Mikoa, hivyo mafunzo hayo yatawawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi na kuchangia katika kupunguza na hatimaye kutokomeza vitendo hivyo katika skuli na jamii kwa ujumla.
Naye Mwakilishi wa UN Women, Ndugu Lucy Tesha, ameipongeza Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kwa namna ilivyolipokea na kulielewa kwa haraka suala la kupambana na ukatili dhidi ya wanawake na wasichana.
Amesema utayari huo unatoa fursa nzuri ya kuimarisha ushirikiano kati ya Wizara na wadau mbalimbali na kurahisisha kufikiwa kwa malengo yaliyowekwa katika mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.
Imetolewa na Kitengo cha Habari, Mawasiliano na Uhusiano – WEMA.