
Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar imekutana na Kamati ya Elimu na Ustawi wa Jamii ya Baraza la Wawakilishi kwa ajili ya kupitia rasimu ya Sheria ya Elimu ya mwaka 2026, inayopendekezwa kufuta Sheria Na. 6 ya mwaka 1982 na kuweka mfumo mpya wa kisheria unaoendana na mahitaji ya sasa ya sekta ya elimu.
Akifungua mafunzo ya siku mbili yaliyofanyika katika Ofisi za Wizara, Mazizini, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Mhe. Lela Muhamed Mussa, alisema Serikali imeamua kuandaa sheria mpya ili kuendana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia, mageuzi ya mitaala, mbinu za ufundishaji pamoja na mahitaji ya soko la ajira na maendeleo ya jamii.
Alisema rasimu hiyo inalenga kuweka msingi imara wa utoaji wa elimu bora, jumuishi na inayozingatia viwango vya kitaifa na kimataifa, huku ikijibu changamoto zinazoikabili sekta ya elimu na kuimarisha usimamizi wake.
Aidha, Mhe. Lela alisema sheria mpya inatarajiwa kuchukua nafasi ya Sheria Na. 6 ya mwaka 1982, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ya kuzifanyia mapitio sheria zilizopitwa na wakati ili ziendane na mazingira ya sasa.
Aliwataka wajumbe wa Kamati ya Elimu na Ustawi wa Jamii kuichambua rasimu hiyo kwa kina ili kuhakikisha sheria itakayopitishwa inazingatia maslahi ya wananchi na kuchangia maendeleo endelevu ya sekta ya elimu Zanzibar.
Akiwasilisha rasimu ya Sheria ya Elimu ya mwaka 2026, Mwanasheria wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Ummulkulthum Rafii Suleiman, alisema sheria hiyo inapendekezwa kuwa na vifungu 62 vinavyolenga kuimarisha usimamizi wa sekta ya elimu, ikiwemo masharti kuhusu uteuzi wa Kamishna wa Elimu pamoja na maeneo mengine muhimu ya kiutawala na kitaaluma.
Kwa upande wake, Mjumbe wa Kamati ya Elimu na Ustawi wa Jamii ya Baraza la Wawakilishi, Mhe. Seif Hamad Suleiman, alisema Kamati itaendelea kuichambua rasimu hiyo kwa umakini ili kuhakikisha sheria mpya inalinda maslahi ya wanafunzi, walimu, wazazi na wadau wote wa elimu, sambamba na kuweka mazingira bora ya maendeleo ya sekta hiyo nchini.
Kupitia mchakato huo, Serikali inalenga kuipatia Zanzibar sheria ya kisasa itakayowezesha utoaji wa elimu bora, jumuishi na yenye kuendana na kasi ya maendeleo ya dunia.