Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Mheshimiwa Lela Muhamed Mussa, leo tarehe 9 Februari 2026 amefungua rasmi Programu ya ufundishaji wa Mtaala wa Cambridge katika Skuli ya Leera International School, iliyopo Mbweni, Mkoa wa Mjini Magharibi – Unguja.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mheshimiwa Waziri amesema kuanzishwa kwa mtaala wa Cambridge kunadhihirisha dhamira ya skuli hiyo katika kuwaandaa wanafunzi kukabiliana na mahitaji ya dunia inayobadilika, huku ikiendelea kuzingatia misingi imara ya maadili ya elimu.
Amesema mtaala huo unalenga kukuza maarifa, fikra pevu, udadisi, kujitegemea katika kujifunza pamoja na nidhamu, uwajibikaji na uadilifu.
Aidha, Waziri amewasisitiza wanafunzi wanaosoma chini ya mitaala ya Cambridge na NECTA kufahamu kuwa wote ni wanafunzi wa jamii moja, na kwamba lengo kuu la mitaala yote ni kujenga wanafunzi wenye maarifa, nidhamu, maadili na uwajibikaji, kwani elimu siyo mitihani pekee bali pia ni tabia, stadi na thamani za maisha.
Kwa upande wake, Mwalimu Mkuu wa Cambridge Wing wa Skuli ya Leera, Ndg. Ramadhan Kusaga, ameishukuru Wizara ya Elimu, Bodi ya Skuli pamoja na Kamati ya Wazee kwa ushirikiano wanaoendelea kuutoa, akiahidi kuwa skuli itaendelea kutoa elimu yenye viwango vya kimataifa, ubora wa kitaaluma na inayozingatia maadili, huku ikijumuisha njia mbalimbali za ujifunzaji.
Naye mwanafunzi Eli Proctor, akizungumza kwa niaba ya wanafunzi wenzake, amesema uzinduzi wa Programu ya Cambridge sambamba na Mtaala wa NECTA ni hatua muhimu kwa skuli hiyo, kwani utaimarisha uwezo wa kufikiri kwa kina, nidhamu, ubunifu na uelewa wa kimataifa, na kuahidi kuwa wanafunzi watakuwa mabalozi wazuri wa programu hiyo.
Skuli ya Leera International School pia inaendesha shughuli za ziada za kielimu kupitia klabu mbalimbali ikiwemo michezo, lugha na urafiki wa kimataifa, kwa lengo la kukuza maendeleo ya wanafunzi kitaaluma, kijamii na kimaadili.
Imetolewa na Kitengo cha Habari, Mawasiliano na Uhusiano – WEMA.